Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa akizungumza waandishi wa gazeti la Mwananchi katika mahojiano maalumu ofisini kwake Makao Makuu ya chama hicho, jijini Dar es Salaam wiki iliyopita. Picha na Edwin Mjwahuzi

“Kushushwa juu ya  fuso na mabomu kwenye kebini umebaki peke yako watu wote wamekimbia. Ndiyo wamekimbia...nimebaki na mlinzi wangu tu pale juu ya gari. Polisi walipoona vile walinifuata na kunirushia mabomu ya machozi na kunifanya nishindwe kupumua kwa dakika tano mfululizo.”
Hii ni sehemu ya ushuhuda wa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kuhusu  misukosuko ya maisha yake kisiasa.
Ni sehemu ndogo iliyojaa taswira ya ukatili, lakini pia nguvu ya ushindi katika harakati za kawaida za kuleta mapinduzi.
Kwa wengi wanaomfahamu Dk Slaa na mambo ambayo hukumbana nayo huenda wasiupe uzito ushuhuda huo, lakini kwa kiongozi huyo machachari aliyegombea urais mwaka 2010 na kushindwa na Rais Jakaya Kikwete wa CCM, hilo ndiyo tukio ambalo anasema hatalisahau katika maisha yake yote kwa sasa.
 “Baadaye nikamwambia mlinzi wangu hebu tuteremke huku juu...na polisi walipoona vile wakatufuata tena na kuendelea kutumiminia risasi, nikaona watatuua.  Vijana wangu walipoona vile wakaniambia Dokta ruka!
”Sasa narukaje kutoka kwenye kebini hadi chini? hapa mimi nikawaeleza nitateremka vipi wakaniambia mzee serereka...bahati nzuri nikaserereka na ule mlango na nilipofika nusu wakaniambia ruka.
“Nilipofika katikati nikaruka, kumbe chini ya gari kulikuwa na vijana wawili nao wamejificha pamoja na mlinzi wangu, tukawa wanne.”
Hii ni simulizi ya Dk Slaa wakati akijibu swali aliloulizwa katika mahojiano maalumu na gazeti hili wiki iliyopita kuhusu ni  jambo gani la kusikitisha ambalo hatolisahau kwa umri wake hasa tangu alipotoka  upande wa pili (upadri) kuingia katika siasa.
Anajibu kuwa ilikuwa ni mkutano uliofanyika Novemba 8 kuamkia Novemba 9 mwaka 2011 ambao ulifanyika Arusha wakati Mbunge wa Jimbo hilo, Godbless Lema alipovutana na polisi kuhusu kutoka kwake mahabusu na siku hiyo ilikuwa Lema aachiwe na wananchi walijitokeza kwa wingi mahakamani kusubiri kuachiwa kwake.
Baada ya kuona umati huo polisi wakapeleleza nani anaweza kuondoa umati huu, wakaambiana,  Dk Slaa au Mbowe (Freeman Mbowe- Mwenyekiti wa Chadema aliyekuwa Arusha), wakaona wanipigie simu na mimi nilikuwa chuo kimoja kilichoko Usa River Arusha natoa mada. Nikawaeleza siwezi kuja, wakaniuliza hadi saa ngapi nikawaeleza hadi saa tisa wakakubali wakaniambia tutakusubiri dokta.
Wananchi walikuwa wengi siku hiyo baada ya kusikia kwamba Lema ataachiwa. Nilipofika nilikuta umati mkubwa sana wa watu hadi nikaogopa kwa kuwa sikuwa hata na vipaza sauti, hivyo nikajiuliza nitawahutubiaje wananchi hawa na wanisikie?
Siku hiyo baada ya mvutano wa Lema na polisi hawakuwa wamemleta mahakamani na wananchi walijua yupo wamemfungia, jambo lililozua vurugu lakini nilipofika polisi wakanieleza tuwapeleke wapi wao wakasema tuwapeleke uwanjani.
Mimi, nikawaeleza mleteni Lema hata kama bado mnataka kumshikilia na tukimaliza mtamchukua ili tutulize munkari wa wananchi hawa, mwanzo walikubali, lakini baadaye walikataa na ilipofika saa 11 jioni wakasema hawatamleta hadi kesho yake saa 12.00 asubuhi.
Nikakubali, tukakesha uwanjani hapo wakati mvua kubwa inanyesha, lakini tulipata taarifa kwamba polisi wanajiandaa kutupiga mabomu. Mimi nikawaeleza haiwezekani kwa kuwa wao ndiyo wametuambia tukae hapa, lakini ilipofika saa 11 alfajiri tuliona mabomu yakimiminika watu walikimbia na kubaki mimi na mlinzi wangu.
Baada ya kuteremka nilipanda ndani ya gari na mlinzi wangu nikafunga mlango kwa kutumia bolt, lakini tulivyopandisha kioo kikagoma ikabidi tukae hivyo hivyo hadi saa 12.30
Chini tunawasikia polisi wakisema mshenzi huyu nimempiga risasi tatu za moto, lakini yuko wapi walijua watakuta maiti chini ya gari.
Ilipofika saa 12.30, mimi nikawaambia tushuke chini kwa kuwa watalivuta gari hili hadi kituo cha polisi na watatukamata. Nikafungua mlango na nikawaita askari na kuwaambia polisi wangu mpooooo..... mmoja akaweka sawa silaha yake, lakini kwa kuwa mkuu wake alikuwapo akawazuia. Hakika tukio hili sitolisahau.
Swali: Kuna malalamiko kuwa ruzuku ambayo chama chenu kinapata huwa haifiki katika ngazi ya chini ya chama. Matumizi ya ruzuku hii ni yapi?
 Dk Slaa: Tuliamua kubadili matumizi ya ruzuku hii ambayo tunaipata kutoka serikalini, Sh233 milioni kila mwezi kwa kununua vitendea kazi na kuvipeleka katika majimbo na kanda zetu zilizopo nchi nzima lengo ni kujenga chama kuanzia ngazi ya chini.
Tuliamua kuchukua uamuzi huo baada ya fedha tulizokuwa tukizipeleka kila mwezi kugombaniwa na viongozi,  matokeo yake hazifanyi kazi kama tulivyokusudia.
Leo hii Chadema ina kanda kumi ambazo zote tumezinunulia gari moja na upande wa majimbo nayo tumenunua pikipiki moja nchi nzima, hivyo hayo ndiyo matumizi ya ruzuku.
Kanda na majimbo yanajiendesha kwa kutumia kadi zaidi ya milioni 75 ambazo tumezipeleka nchi nzima, kila kadi ni Sh1500 na ada ni Sh1000, lakini kuna maeneo kadi hii inauzwa kwa Sh10,000 na nilikwenda Mwanza hivi karibuni nikakuta kiongozi wangu kaweka rehani kadi ili akopeshwe fedha. Hii inaonyesha ni jinsi gani kadi hizi zilivyo na thamani.
Swali: Chadema ni moja ya vyama vinavyojipambanua kupambana na ufisadi nchini. Hata hivyo, taarifa zilizopo zinaonyesha kuwa hakijatoa ushirikiano wa mahesabu yake kukaguliwa na CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali). Nini maoni yako juu ya jambo hili?
Dk Slaa: Serikali kwa kukurupuka ilitengeneza sheria na haikutengeneza kanuni. Sisi Chadema tangu mwaka 2007 tunakaguliwa na wakaguzi wa ndani wanaoidhinishwa na Kamati Kuu na Baraza Kuu la Chadema. Baada ya kuona hili mimi nilikwenda ofisi ya Msajili wa Vyama kuuliza kanuni ipo wapi, mpaka leo hii sijajibiwa na ukweli ni kwamba hakuna kanuni ya ukaguzi sasa unakaguliwa na unatoa ripoti katika mfumo upi?
Mwaka 2012, ofisi ya msajili ilituandikia barua kwamba vyama vya siasa vitakaguliwa na vyama vitalipa vyenyewe. Sisi Chadema hatukukubali kwani fedha zinazokaguliwa zimetoka serikalini na mkaguzi wangu wa ndani anatukagua kwa Sh2 milioni, lakini akija mkaguzi tutakaguliwa kwa zaidi ya Sh50 milioni sasa kwa gharama hii hatuiwezi.
Swali: Operesheni yenu ya M4C imefanyika kwa muda mrefu katika mikoa mbalimbali nchini. Je, ni maeneo gani mmegundua ni magumu kwenu kuyapenya na kujiimarisha? M4C imekisaidia vipi chama, kiasi gani kimetumika kuifanikisha?
Dk Slaa: Ngoja niwaeleze, katika operesheni hiyo hakuna eneo ambalo Chadema lilikuwa gumu kwake bali kila eneo lilikuwa ni rahisi na wananchi walituelewa vizuri sana wakati wa mikutano yetu.
M4C imekifanya chama kujipambanua hadi vijijini tofauti na ilivyokuwa mwanzo kwa CCM kutawala nchi nzima lakini leo hii kama ni mpira wa miguu CCM ina wachezaji 11 uwanjani hivyo hivyo na Chadema ina wachezaji 11 na tutaendelea na operesheni hii hadi 2015 katika uchaguzi mkuu.
Swali: Kila uchaguzi mkuu na uchaguzi mdogo wa ubunge kila zinapofanyika chama chenu hulalamika kuwa kuna wizi wa kura unaofanywa  na CCM. Je,  Mmeshagundua wizi huo wa kura unavyofanyika?
Dk Slaa: Afadhali nimeulizwa swali hili kwani watu wanatuona kama Chadema ni walalamikaji tu. Unajua uchaguzi kimsingi ni uwanja wa mpira. Tunapolalamika tunakuwa na hoja.
Mfano katika chaguzi ndogo za Kalenga, Arumeru, tulibaini vituo 20 hewa na  Igunga tulibaini daftari la kudumu la wapigakura kuwa limeboreshwa wakati tangu uchaguzi wa mwaka 2010 tunajua kuwa daftari hili halijafanyiwa marekebisho yoyote sasa kwa njia hii ndivyo ambavyo CCM imekuwa inaiba na njia hiyo hiyo hadi katika uchaguzi mkuu wanavyofanya.
Swali: Baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 mlitangaza kwamba hamtashirikiana na Rais Jakaya Kikwete kuonyesha kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa rais. Lakini hivi sasa mnaonekana kushirikiana naye katika mambo mbalimbali. Je mlibadili uamuzi wenu?
Dk Slaa: Kuna tofauti kati ya kumtambua na kufanya kazi na mtu, kuna rais mwingine Ikulu.... kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania akishatangazwa rais huwezi kubadili, tunafanya naye kazi kwa kuwa hakuna jinsi lakini unaweza kuwa rais kisheria, lakini siyo kisiasa.
Tunafanya kazi na Rais (Kikwete) kwa kuwa hakuna jinsi na ndiyo maana hata yeye anajua haendi katika mambo ya kawaida kwa wananchi hadi unapofika wakati wa kwenda kufungua tu miradi lakini kisheria ni Rais halali.
Swali: Utamkumbuka kwa jambo gani Rais Kikwete katika uongozi wake?
Dk Slaa: Sina la kumkumbuka Kikwete. Hakuna jambo lolote alilolifanya litakalonifanya nimkumbuke zaidi ya kuzidisha ugumu wa maisha tu kwa Watanzania.
Leo hii Watanzania wanalala bila kupata mlo hata mmoja, huduma za afya, maji na elimu bado imekuwa tatizo sasa kwa hali hiyo mimi nimkumbuke kwa lipi? Sina la kumkumbuka.
Kipindi alipoingia madarakani mwaka 2005 alikuwa na kaulimbiu ya  nguvu mpya, ari mpya na kasi mpya lakini leo hii yeye mwenyewe kaulimbiu yake ameikimbia, sasa mimi nimsifu au nimkumbuke kwa lipi katika uongozi wake?
 Swali: Wabunge wa NCCR-Mageuzi, David Kafulila na Felix Mkosamali walikuwa wanachama wenu, lakini baadaye waliondoka kutokana na kutoelewana na baadhi ya viongozi. Je, chama kinasikitika kuondoka kwao? Wakiamua kurudi mtawapokea?
Dk Slaa: Huwezi kumzuia mtu kuchukua uamuzi wowote anaoupenda, kama Chadema hatukujuta kuondoka kwao kwani ndivyo siasa ilivyo.
Katika siasa hakuna urafiki wa kudumu na hakuna uadui wa kudumu hivyo wakiamua kurejea tutawapokea.
Swali: Ni jambo gani ambalo linakufurahisha tangu uwe Katibu Mkuu wa Chadema?
Dk Slaa: Nafurahi kuona  kwamba Watanzania wa sasa siyo wale wa miaka ya nyuma kabla ya vyama vingi vya siasa. Leo hii kila mmoja anajua haki yake lakini pia kuidai na kuitetea yenye mwenyewe.
Hali ya Watanzania kujua haki zao haikuja hivi hivi tu kwani baadhi  wamepigwa sana, wamepoteza mali zao, wamepigwa mabomu, wamefilisika na wengine wamepoteza maisha yao. Hivyo jambo hili kweli mimi ninafarijika na wabunge wengi wa CCM linawaumiza sana wanaposikia maandamano.
Kiongozi yoyote wa siasa furaha yake ni pale anapoona mafanikio yanaonekana hasa fikra na tabia kwa wananchi. Watanzania walikuwa waoga, lakini leo wanaweza kusimama na kusema.  Leo hii unaona katika televisheni, wanawake unapofika wakati wa kudai haki za ardhi wanavyolalamika tofauti na awali walikuwa kimya.
Swali: Imekuwa kawaida kuwapokea wanachama wanaoachwa na CCM. Je, ikitokea wanasiasa wakongwe wa CCM kama Frederick Sumaye au Samwel Sitta ambao wamekuwa wakitajwatajwa kuwania urais kupitia chama hicho, ikitokea wakatoswa huko Je, mtawapokea?
Dk Slaa: Aah....Hapo awali tulikuwa tukiwapokea kwa kuwa tulikuwa hatujajiimarisha zaidi na tulikuwa na lengo la kujiimarisha zaidi katika baadhi ya maeneo lakini leo hii tumekamilika kila nyanja hivyo hatutapokea tena masalia yanayoachwa na  CCM.
Swali: Mara kwa mara wabunge wenu waliopo katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wanaposhindwa kukubaliana na jambo fulani ambalo wanajua halina masilahi kwa wanachama au taifa hutoka nje ya Bunge. Je, hatua hiyo imekisaidia chama? Maeneo gani?
Dk Slaa: Wabunge wetu wanapotoka nje siyo kwamba wanatoka kwa kupenda bali wanatoka kisheria lakini pia ni kupinga mabavu yanayotumika na CCM kutokana na wingi wao.
Katika jambo hili huwezi kusema kwamba kutoka kwao kunakisaidia chama bali kinafikisha ujumbe kwa watawala juu ya matumizi mabaya wingi wao bungeni kuwakandamiza wananchi na sisi tutaendelea kutoka pale tunapoona masilahi ya wananchi wanaminywa na kuporwa na wachache, tutapinga kwa hoja na ikishindikana tutatoka.
Swali: CCM imekuwa  ikidai ina mtaji wa wanachama zaidi ya milioni 5, ninyi mna wanachama wangapi?
Dk Slaa: Nina taarifa ya mkaguzi akiwataka CCM kutoa idadi ya wanachama wao lakini hawakutoa, kama wana idadi hiyo watoe, taarifa ya CCM ya mwaka 2010 inaonyesha walikuwa wanapata Sh9 bilioni kama ada za kadi lakini sasa imeshuka hadi Sh2 bilioni, sasa kwa hali hiyo si idadi hiyo imeshuka?
Sitakupa idadi kuwa Chadema tuna wanachama wangapi, kwani tuko tunaingiza wanachama wetu katika mfumo wa teknolojia na sasa tuna ‘data bank’ kila jimbo na kanda utakapokamilika nitawaeleza tuna wanachama wangapi lakini uongo wa CCM hauna ukweli wowote.
Swali: Mchakato wa Katiba mpaka hapa ulipofikia ni nani wa kuunusuru?
Dk Slaa: Mwenye rungu la kutegua kitendawili hiki ni Rais Kikwete na si mtu yeyote kutoka ndani au nje ya nchi.
Rais Kikwete ndiye aliyeisaini Rasimu ya Katiba na kuipeleka bungeni ijadiliwe na ipitishwe lakini ni yeye mwenyewe alipokwenda kulizindua Bunge hilo akavaa kofia ya Umwenyekiti wa CCM na kuuvuruga kutokana na kutoa misimamo yake.
Rais Kikwete achukue nafasi yake kama mkuu wa nchi. Rais wa nchi hapaswi kuwagawa Watanzania lakini pia wakati wa mchakato wa Katiba Rais  hatakiwi kuonyesha msimamo wake hivyo achukue hatua za kuurejesha katika reli ili uweze kuendelea.
Swali: Bunge la Katiba linatarajiwa kuanza Agosti 5 mwaka huu na Jaji Warioba na viongozi wa dini wamewashauri mkutane na kuondoa tofauti na CCM, pia mrejee bungeni, haya mmeyapokeaje?
Dk Slaa: Viongozi wetu wa dini tunawapenda sana.  Maaskofu wanatakiwa kuma makini kabla ya kutoa kauli hizo kwani mwisho wa siku zitakuja kuwahukumu.
Maaskofu wangu hawajui kilichopo bungeni, hoja yetu ni je, tunarudi tutajadili rasimu iliyopo mezani? Hatuwezi kukubali kuona rasimu ikichakachuliwa nasi tukakubali.
Viongozi wangu wa dini nawapenda sana ila nawasihi wasiingie katika hili kwani litakuja kuwahukumu siku ya mwisho kwa kutoa kauli ambazo hawajazifanyia utafiti
Swali: Baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 CUF waliungana na CCM na kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar, nanyi Chadema mliwaita CCM B lakini leo mmeshirikiana na kuunda Ukawa Je, UCCM B unauzungumziaje?
Dk Slaa: Kama nilivyosema hapo mwanzo kwamba katika siasa hakuna urafiki wa kudumu na hakuna uadui wa kudumu. Sisi na CUF tulitofautiana katika malengo lakini sasa tumekaa na kuona malengo yao na yetu yanafanana ndiyo maana tukaona tuunganishe nguvu katika jambo hili la kitaifa.
Swali: Kuna uwezekano Katiba Mpya isipatikane mwaka 2015 mwaka ambao kutafanyika uchaguzi mkuu. Je, kipi kifanyike ili uchaguzi huo uwe wa huru na haki?
Dk Slaa: Hata kama ikipatikana Machi au Aprili mwakani bado haiwezi kutumika katika uchaguzi huo kwani kutakuwa na utaratibu wa kufumua sheria zote hizo ili zifanye kazi, jambo ambalo haliwezi kutekelezeka kwa kipindi kifupi.
Kinachotakiwa kufanyika ni kufanya  marekebisho ya Katiba ya sasa ya mwaka 1977 katika vipengele viwili vya Tume Huru ya Uchaguzi na Rais atachaguliwa na nusu ya idadi ya wapiga kura wote.
Swali: Je, Katika uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2015 utagombea tena urais?
Dk Slaa: .....Siwezi kulizungumzia suala hili kwani kazi niliyopewa ndani ya chama hiki kama Katibu Mkuu ni kukijenga chama kazi ambayo nimeifanya hadi ngazi ya vijiji nchi nzima. Hivyo ukiniuliza swali hili nitakuwa sina jibu lolote zaidi ya kukueleza kuwa kazi niliyopewa nimeitekeleza na naendelea kuitekeleza kwa mafanikio makubwa.
Katika historia ya nchi hii hakuna kiongozi yeyote mkubwa wa chama aliyezunguka nchi nzima, lakini wilaya zote za Tanzania nimepita kwani nilikuwa nimebakiza wilaya ya Ngara ambayo nayo nimefika katika ziara ya Ukawa, hivyo haya ndiyo mafanikio na jambo la urais kwangu silifikirii kabisa.
MWANANCHI

0 comments:

Post a Comment

 
Top